Tanzania emblem

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Habari

WAZIRI SIMBAWENE; MFUMO WA KIELEKTRONI NI USHINDI KATIKA KUTENDA HAKI


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe.George  Simbachawene amesema kitendo cha  Serikali kuanza kutumia mfumo wa kielektroni wa Kukusanya, Kuchakata na Kutunza Kumbukumbu za Kesi Jinai (CMIS) ni ushindi katika utendaji haki kwa umma.

Mhe. George Simbachawene amesema hayo leo Jijini Dodoma  kwenye uzinduzi wa mfumo huo uliosanifiwa na kutengenezwa na Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) kwa kushirikiana na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka.

"Mfumo huo umekamilika katika wakati sahihi ambapo Rais  Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anaendelea na jitihada za kuimarisha utoaji haki kwa wananchi" ameongeza.

Vile vile, amebainisha kuwa  mfumo huu umeunganishwa na mfumo unaowezesha mifumo ya Serikali kuwasiliana na  kubadilishana taarifa (GovESB).

Amesema mifumo ya Taasisi za Haki Jinai kama vile Polisi, TAKUKURU  na Mahakama imeunganishwa na inabadilishana taarifa ikiwa ni  utekelezaji wa  maelekezo ya Rais  Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhusu mifumo ya Serikali kubadilishana taarifa.

Aidha, Mhe. Simbachawene  ametumia fursa hiyo kuzihimiza Taasisi zote za Umma kutekeleza jitihada za serikali mtandao kwa kasi ili kurahisisha na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa umma.

Naye, Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Pauline Gekul, amesema Wizara ya Katiba na Sheria  imejizatiti kutekeleza jitihada za Serikali mtandao kwa kutengeneza mifumo madhubuti ya TEHAMA ili kutoa huduma bora kwa umma.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw. Xavier Daudi amesema kuzinduliwa kwa mfumo huo ni hatua kubwa katika kuhakikisha haki inatendeka kwa wananchi kwani jambo hilo halikuwa rahisi kufanyika kwa siku za nyuma.

‘’Mfumo huu unafungua ukurasa mpya katika kuelekea uchumi wa kidijitali huku tukifanikisha azma ya. Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha mifumo yote ya utoaji haki inawasiliana ‘’ amesema Bw. Daudi.

Awali, Mkurugenzi wa Mashtaka, Sylvester Mwakitalu, amesema mfumo huo utatunza kumbukumbu zote ikiwamo hati za mashtaka na hukumu  na utakuwa na uwezo wa kuonesha mzunguko wa jalada kwa uwazi.

Kadhalika, Mkurugenzi Mkuu wa eGA, Mhandisi Benedict Ndomba, amesema kuzinduliwa kwa mfumo huo ni utekelezaji wa dhamira ya Serikali ya kuboresha mifumo ya utendaji kazi Serikalini.