Tanzania emblem

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Habari

WAZIRI SIMBACHAWENE: USHINDANI WA  AJIRA KATIKA UTUMISHI WA UMMA NI JAMBO LISILOEPUKIKA KWA SASA 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.George Simbachawene amesema suala la ushindani katika  upatikanaji wa ajira katika Utumishi wa Umma ni jambo lisiloepukika kutokana na idadi kubwa ya wasomi iliyopo kwa sasa 

Amesema dhamira hiyo ya kuhakikisha waombaji kazi wote wanafanya usaili kunasaidia  kuwapata watumishi wenye sifa stahiki katika utumishi wa umma na kuondoa dhana ya upendeleo iliyokuwa imejengeka miongoni mwa watu


Mhe. Simbachawene ametoa kauli hiyo alipotembelea kituo cha usaili wa kada ya Ualimu  Mkoani  Singida ili kujionea mwenendo wa zoezi hilo,  ikiwa ni utekelezaji wa Sera ya Menejimenti na Ajira katika Utumishi wa Umma ya Mwaka 2008 na Sheria ya Utumishi wa Umma Sura 298 inayoelekeza  kuwa ajira katika utumishi wa umma  zipatikane kwa ushindani

"Hakuna palipoandikwa kuwa watu wote waliosoma wataajiriwa na Serikali ndio maana ajira za serikali ni za  ushindani kwani waliosoma  ni wengi lakini nafasi ni chache.

Amesema Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma mara baada ya kutangaza kazi za  Ualimu, waombaji   201,707 walijitokeza kuomba  lakini baada ya mchujo kutokana na baadhi kutokukidhi vigezo ikiwemo kutokuweka  baadhi ya vyeti kama ilivyoelekezwa walichujwa  hadi kufikia waombaji 107,746

Hata hivyo,  Mhe.Simbachawene ametumia fursa hiyo kuwasihi waombaji kazi kuhakikisha wanaweka vyeti vyao vinavyotakiwa ili kuepuka na mchujo katika hatua za  awali.

Usaili wa kada ya Ualimu unaendelea katika vituo mbalimbali nchi nzima na utakamilika  Februari 24 Mwaka huu.