Habari
WAZIRI KIKWETE AFUNGUA MKUTANO WA 13 WA KAMATI TENDAJI YA SHIRIKISHO LA MAMLAKA ZA KUPAMBANA NA RUSHWA BARANI AFRIKA ATAJA MAENEO MANNE YATAKAYOSAIDIA KUKABILIANA NA RUSHWA
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema ili Afrika iweze kuwa na uwezo uliojitosheleza ni lazima kuwe na azimio endelevu la pamoja la kukabiliana na rushwa.
Mhe. Kikwete ameyasema hayo leo tarehe 13 Aprili, 2026 wakati akifungua Mkutano wa 13 wa Kamati Tendaji ya Shirikisho la Mamlaka za Kupambana na Rushwa Barani Afrika ulioanza leo katika Hoteli ya Forest Hill jijini Arusha.
Waziri Kikwete ameainisha maeneo manne ya kuchukua hatua za makusudi za kukabiliana na rushwa Barani Afrika ikiwemo kuendelea kuimarisha ushirikiano mipakani kwani rushwa imekuwa ni tatizo la kimataifa ambalo linahusisha mtiririko wa fedha haramu na masuala ya kimtandao, huku akisisitiza kubadilishana habari katika maeneo ya urejeshaji wa mali na uchunguzi wa kifedha.
Amesema ni lazima kukubali kuwa teknolojia ina nguvu katika kukuza uwazi na kupunguza mianya ya rushwa ambapo mifumo ya kidijiti imeongeza uwajibikaji kwa kiasi kikubwa katika ununuzi wa umma, ukusanyaji wa mapato na utoaji wa huduma .
Amesisitiza kuwa ni lazima kukuza uongozi wa kimaadili na uadilifu katika ngazi zote za kijamii kwani vita dhidi ya rushwa huanza na maadili ambayo lazima yaonekane katika utumishi wa umma na tabia binafsi.
Aidha, ameongeza kuwa ni muhimu kushirikisha wananchi, mashirika ya kiraia, na sekta binafsi kama washirika hai katika mapambano dhidi ya rushwa kwani suala hili sio la mtu mmoja au taasisi moja pekee.
Amesema rushwa ni kikwazo katika utoaji haki na huduma muhimu kama vile afya, elimu na miundombinu kwa wananchi wa kawaida, vilevile ni tishio katika mabadiliko ya kiuchumi na inapunguza kasi ya maendeleo katika mataifa yetu.
“Ni imani yangu kwamba mkutano huu utatumika kama jukwaa muhimu la kuimarisha ushirikiano, kubadilishana uzoefu, na kuimarisha azimio letu la pamoja katika kushughulikia mojawapo ya changamoto sugu zinazoendelea kuikabili Afrika,” Mhe. Kikwete amesisitiza.
Amesema katika kupambana na rushwa, Tanzania chini ya uongozi wa Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, imekuwa na dhamira thabiti ya kuendeleza uwazi, uwajibikaji na utawala bora kwa kuimarisha mifumo ya kisheria na kitaasisi, mifumo ya usimamizi wa fedha za umma na kuboresha utoaji wa huduma katika sekta zote,” Mhe. Kikwete amesisitiza.
Ameongeza kuwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ina jukumu muhimu katika kutekeleza ajenda ya kitaifa ya kupambana na rushwa kwa kuhakikisha rasilimali za umma zinasimamiwa kwa manufaa ya wananchi wote.
Amesema kwa pamoja, tunaweza kuijenga Afrika inayofafanuliwa si kwa rushwa, bali kwa uadilifu, si kwa fursa zilizopotea, bali kwa mafanikio ya pamoja, si kwa mifumo dhaifu, bali na taasisi imara na zinazoaminika. Mkutano huu ukaashirie hatua nyingine muhimu kuelekea siku zijazo.
Akitoa neno la utangulizi, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Bw. Crispin Chalamila, amesema lengo la mkutano huo ni kujadili na kubadiliashana uzoefu kuhusu namna bora ya kukabiliana na rushwa ambalo ni tatizo kubwa katika Bara la Afrika. “Tutabadilishana uzoefu kwani tunatamani rushwa itokomezwe kabisa katika Bara la Afrika,” amesisitiza.
Wajumbe wa Kamati Tendaji ya AAACA ni Wakuu wa Mamlaka za Kuzuia na Kupambana na Rushwa kutoka Nchi 9 Wanachama ambazo ni Egypt, Mali, Cameroon, Congo Brazaville, Algeria, SieraLeone, Burundi, Zimbabwe pamoja na Tanzania.
