Habari
WATUMISHI OFISI YA RAIS WASISITIZWA KUWA DARAJA SIO UKUTA

Utoaji wa huduma bora kwa wateja ni matokeo ya uwekezaji unaofanywa na menejimenti ya taasisi katika maeneo mbalimbali mathalani ya rasilimaliwatu, mifumo na miundombinu ambayo huleta tija kwa haraka.
Amesema, taasisi hufanya uwekezaji mkubwa kwa lengo la kubadili mtazamo na fikira za watumishi katika utendaji kazi ili waweze kuwa daraja na sio ukuta kwa kuwa wananchi wanatafuta huduma bora kwa haraka, wakati na gharama nafuu.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Mafunzo kutoka Chuo cha Diplomasia - Uchumi (Economic Diplomacy Training Institute) Bw. Lucas Jackson Septemba 22, 2025 wakati akitoa mafunzo ya namna bora ya kuhudumia wateja yaliyofanyika katika Jengo la Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Mtumba Jijini Dodoma.
“Wateja hulalamika kwa sababau ya kukosa huduma bora, hivyo moja ya majukumu ya menejimenti katika taasisi ni kuweka mazingira bora ya utoaji huduma kwa wateja na watumishi wanawajibika kuona umuhimu huo na kutoa huduma ipasavyo” alisema Bw. Lucas.
Aidha, amewaelekeza watumishi wa ofisi hiyo kupunguza urasmu ili wateja waweze kuwafikia kwa urahisi na kuondoa malalamiko. Ameongeza kuwa, malalamiko mengi na hasira za Wateja hutokana na watumishi kuwa na ahadi zisizotimilika na kutotoa mrejesho kwa wakati. Hivyo, ametoa somo la namna ya kuwasiliana na wateja na kuwafanya waridhike na huduma.
Naye, Kaimu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-UTUMISHI Bw. Cosmas Ngangaji amemshukuru Bw. Lucas kwa kutoa mafunzo sahihi na kwa wakati muafaka ambapo watumishi wamepata elimu na kuongeza ujuzi wa namna ya kuwahudumia watumishi wengine kutoka taasisi mbalimbali na wananchi kwa jumla.
“Ninaamini utulivu na usikivu ambao nimeuona wakati wote wa wasilisho la Bw. Lucas ni ishara tosha kuwa soma limeeleweka bayana na mtaishi kwa vitendo mafunzo hayo wakati wa utumishi na kuwahudumia wananchi” alisema Bw. Ngangaji.
Vilevile, amesisitiza na kuwataka watumishi hao kuzingatia mafunzo hayo na kuyaishi kwa vitendo kwa kuwa utulivu wao katika kufuatilia mafunzo ulikuwa mkubwa na muwezeshaji ameeleza kwa ufanisi mkubwa.
Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imekuwa na utaratibu wa kutoa mafunzo kwa watumishi wake kila Jumatatu ya wiki kwa lengo la kuwajengea uwezo zaidi.