Tanzania emblem

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Habari

WARATIBU NA WAELIMISHA RIKA WAPATIWA MAFUNZO YA KUTEKELEZA AFUA ZA KUDHIBITI VVU NA UKIMWI


Ofisi ya Rais-UTUMISHI kupitia Idara ya Uendelezaji Sera imetoa mafunzo kwa waratibu na waelimisha rika wa Wizara, Mikoa na Taasisi za umma kwa lengo la kuwajengea uwezo na stadi za utekelezaji wa afua kwa ajili ya kuwalinda watumishi wa umma dhidi ya VVU na Ukimwi.

Katika mafunzo hayo Mkurugenzi Msaidizi Anuai za Jamii na Mratibu wa VVU, Ukimwi na Magonjwa Yasiyoambukiza, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Mwanaamani Mtoo amesema Ofisi ya Rais-UTUMISHI inaungana na Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika jitihada za kutokomeza VVU na Ukimwi ili kuendelea kuwa na nguvukazi hususani katika utumishi wa umma yenye afya njema ili iweze kutoa huduma bora kwa wananchi.

Bi. Mtoo ameongeza kuwa mafunzo haya ni endelevu kwa kuwa ni sehemu ya mapambano dhidi ya VVU na Ukimwi ili kuwalinda watumishi wa umma na kuhakikisha taifa linaondokana na vifo vitokanavyo na Ukimwi ifikapo mwaka 2030.

“Tunatoa mafunzo haya kwa waratibu na waelimisha rika wa Wizara, Mikoa na Taasisi wakati wa maadhimisho ya Siku ya Ukimwi ili waende kutoa elimu ya kudhibiti VVU na Ukimwi mahali pa kazi katika Utumishi wa Umma” amefafanua Bi. Mwanaamani.

Naye, mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo ambaye ni Mratibu wa VVU na Ukimwi kutoka Hospital ya Rufaa ya Tumbi-Pwani, Dkt. Hapiness Ruta ameishukuru Ofisi ya Rais-UTUMISHI kwa kutoa mafunzo hayo ya VVU na Ukimwi na kuahidi kuyafanyia kazi ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa watumishi wa umma waliopo katika maeneo yao ya kazi.

Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, kupitia Idara ya Uendelezaji Sera ipo mkoani Morogoro kwenye Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani yanayofanyika kitaifa mkoani humo kuanzia tarehe 24 Novemba hadi tarehe 02 Disemba, 2023. Kaulimbiu ya maadhimisho hayo ni Jamii iongoze kutokomeza Ukimwi.