Habari
WAJUMBE WA KAMATI YA KUDHIBITI VVU/UKIMWI NA MSY WASISITIZWA KUTEKELEZA MAJUKUMU YAO KIKAMILIFU
Mwakilishi wa Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bi. Leila Mavika amewaelekeza Wajumbe wa Kamati ya Kitaifa na waratibu ngazi ya Wizara, Taasisi zinazojitegemea, Wakala za Serikali, Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kutekeleza majukumu yao kwa weledi ili kujenga Utumishi wa Umma wenye afya, tija na unaoendana na matarajio ya wananchi.
Bi. Mavika ameyasema hayo leo tarehe 02 Machi, 2026 wakati akifungua kikao kazi cha kupokea taarifa ya utekelezaji wa Afua za kudhibiti VVU, UKIMWI na magonjwa Sugu Yasiyoambukiza ya kipindi cha robo ya pili ya Mwaka wa fedha 2025/2026 ngazi ya Mkoa na Taifa.
Aidha Bi. Mavika amezipongeza Taasisi za Umma ambazo zimekuwa zikifanya vizuri katika kusimamia afua za VVU, UKIMWI na MSY hasa kwenye Kuratibu kampeni za upimaji wa hiari wa VVU na utoaji wa elimu ya lishe bora, mazoezi na afya ya akili.
“Haya mafanikio ni ya kujivunia, lakini bado tunayo safari ya kwenda kufikia malengo tuliyojiwekea pamoja na mafanikio hayo” Bi. Mavika alisema.
Vilevile Bi. Mavika amesisitiza kuwa ushirikiano wa Wadau na Taasisi simamizi za Kudhibiti VVU UKIMWI na Magonjwa Yasiyoambukiza ikiwemo Wizara ya Afya, Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS), na wadau wengine ni muhimu katika kuhakikisha utekelezaji wa afua hizo unaendana na miongozo ya kitaifa.
Amehitimisha kwa kuwataka Wajumbe wa Kamati ya Kitaifa na waratibu kutekeleza majukumu yao kwa weledi kwa kuweka vipaumbele vinavyoendana na hali halisi ya watumishi na kuhakikisha kuwa kila taasisi ina mpango kazi unaotekelezeka.
Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi Anuai za Jamii na Mratibu wa VVU, UKIMWI na Magonjwa Yasiyoambukiza, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Mwanaamani Mtoo amemshukuru Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-UTUMISHI kwa utayari wake katika utekelezaji wa majukumu yaliyokasimiwa katika kuimarisha afya na ustawi wa Taifa.
Naye Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Kagera Bw. Bwai Biseko akizungumza kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera, amewashukuru waratibu kwa namna ambavyo wameshiriki kikamilifu katika kikao hicho na kutoa wito kwa kila mshiriki kuzingatia na kutekeleza yote yaliyoshauriwa.
