Habari
PROF. SHEMDOE AZITAKA TAASISI ZA UMMA KUIMARISHA MATUMIZI YA MIFUMO YA KIDIJITI
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Prof. Riziki Shemdoe amezitaka taasisi zote za umma nchini kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidijiti ili kuboresha utoaji wa huduma kwa Wananchi, kuongeza uwajibikaji na kuimarisha ufanisi katika utumishi wa umma.
Prof. Shemdoe ametoa kauli hiyo Juni 23, 2026 jijini Dodoma wakati akimwakilisha Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka, katika kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyofanyika katika Viwanja vya Chinangali Park.
Alisema, matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yamekuwa nguzo muhimu katika kuimarisha utendaji wa Serikali kwa kurahisisha upatikanaji wa huduma, kuongeza uwazi na kupunguza gharama za utoaji wa huduma kwa wananchi.
Prof. Shemdoe alibainisha kuwa maadhimisho ya mwaka huu yamehusisha Taasisi 226 za umma zilizotoa huduma mbalimbali kwa wananchi, zikiwemo huduma za hati za viwanja, vyeti vya kuzaliwa, vitambulisho vya Taifa, huduma za afya za kibingwa pamoja na huduma mbalimbali za kiutumishi.
“Utaratibu huu wa kuwaletea Wananchi huduma karibu nao ni mzuri na unapaswa kuendelezwa kwa kuwa unarahisisha upatikanaji wa huduma, kuimarisha mawasiliano kati ya Serikali na Wananchi na kuongeza imani ya wananchi kwa Serikali yao,” alisema Prof. Shemdoe.
Katika hafla hiyo, Prof. Shemdoe alizindua mifumo ya GSD na NGAO inayolenga kuboresha utoaji wa huduma za Serikali na kuimarisha usalama wa mifumo ya kidijiti.
Alieleza kuwa mfumo wa GSD utawawezesha wananchi kupata huduma mbalimbali za Serikali kupitia dirisha moja kwa urahisi na kwa wakati, huku mfumo wa NGAO ukiimarisha usalama wa taarifa za Serikali kwa kutumia teknolojia ya uthibitishaji wa vipengele vingi (Multi-Factor Authentication).
Aidha, aliielekeza Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) kuendelea kusimamia uunganishaji wa mifumo ya Serikali ili kuhakikisha Taasisi za Umma zinabadilishana taarifa kwa ufanisi, kupunguza urudufu wa taarifa na kuongeza tija katika utoaji wa huduma.
Vilevile, Prof. Shemdoe aliagiza kufanyika kwa tathmini ya maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma kwa kipindi cha miaka mitatu iliyopita ili kubaini mafanikio yaliyopatikana, changamoto zilizojitokeza na kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha maadhimisho yajayo.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – UTUMISH, Bw. Juma Mkomi, alisema maadhimisho hayo yamelenga kuimarisha uwajibikaji, uwazi na ubora wa huduma kwa wananchi kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa zinazowezesha utoaji wa huduma kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.
Aliongeza kuwa maadhimisho hayo yameipa Serikali fursa ya kuonesha mafanikio ya uwekezaji uliofanyika katika sekta ya umma, hususan katika matumizi ya TEHAMA ambayo yamechangia kuboresha huduma na kuongeza kuridhika kwa wananchi.
