Tanzania emblem

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Habari

MIPANGO YA TAASISI ITUMIKE KATIKA KUTATUA CHANGAMOTO YA URUDUFU WA MIFUMO YA TEHAMA – Mhe. Kikwete


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amezielekeza taasisi zote za umma kuweka mipango itakayozisaidia kutatua changamoto ya urudufu wa mifumo ya TEHAMA ili kukuza na kuimarisha jitihada za serikali mtandao na kuboresha utendaji kazi katika kutoa huduma bora kwa wananchi kwa lengo la kufikia azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwa na serikali ya kidijitali.

Mhe. Kikwete ametoa maelekezo hayo jijini Arusha wakati akifunga Kikao kazi cha nne cha serikali mtandao kilichowashirikisha wadau zaidi ya 1300 wa serikali mtandao nchini.

Changamoto za TEHAMA ili ziweze kufikia mafanikio katika utekelezaji wa jitihada za serikali mtandao, hatua madhubuti zichukuliwe ikiwa ni pamoja na kujiwekea mipango katika taasisi zenu ili changamoto hizo ziweze kutatuliwa,” Mhe. Kikwete amesisitiza.

Aidha Mhe. Kikwete amewataka wataalam wa TEHAMA kushirikiana na Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) katika kutekeleza jitihada za serikali mtandao kupitia msaada na ushauri wa kitaalam unaotolewa na mamlaka hiyo kwa lengo la kila mtumishi kuweza kuijenga serikali ya kidijitali.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Xavier Daudi ameipongeza Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) kwa kutekeleza azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuijenga Tanzania kuwa ya kidijitali kwa kuibadilisha nchi na utumishi wa umma kupitia sera na mbinu mbalimbali za utendaji kazi serikalini ili kutoa huduma bora kwa wananchi kwa kutumia TEHAMA.

Bw. Xavier ameongeza kuwa, kukutana kwa wadau mbalimbali katika kikao kazi hicho kutoka katika Wizara, Taasisi na Mashirika iwasaidie kujadili hali ya utekelezaji wa serikali mtandao katika taasisi za umma zikiwemo changamoto na mbinu za kukabiliana nazo ili kupunguza gharama za uendeshaji wa serikali.

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), Mhandisi Benedict Ndomba amesema kuwa, miradi ya mifumo ya TEHAMA katika taasisi za umma nchini kupitia kaulimbiu ya kikao kazi hicho ikizingatia Sera, Sheria, Kanuni na Miongozo ya Serikali Mtandao katika ujenzi wa miundombinu na mifumo ya TEHAMA itasaidia kupunguza urudufu wa mifumo, kurahisisha taasisi za umma kubadilishana taarifa na kuokoa fedha za umma kwa kudhibiti upotevu wa mapato ya serikali.

Kikao kazi hicho kilichoanza tarehe 06 Februari, 2024 na kuhitimishwa leo tarehe 08 kimebeba kaulimbiu ya “Uzingatiwaji wa Sera, Sheria, Viwango na Miongozo ya Serikali Mtandao kwa Ubadilishanaji salama wa Taarifa”.