Tanzania emblem

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Habari

MHE. SIMBACHAWENE AWATAKA WAAJIRI KUTENGA BAJETI YA WATUMISHI WA UMMA KUSHIRIKI SHIMIWI


 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.George Simbachawene amewataka  Waajiri  kutenga bajeti ya kutosha kwa ajili ya kuwawezesha Watumishi wa Umma  kushiriki Michezo ya SHIMIWI ili kukidhi malengo na misingi ya kuanzishwa  kwa michezo hiyo ili kuleta tija iliyokusudiwa

 

Mhe.Simbachawene ametoa kauli hiyo leo Oktoba 5, 2024 Mkoani Morogoro  wakati akifunga Mashindano ya  38 ya Shirikisho  la Michezo la Wizara na Idara za Serikali Tanzania ( SHIMIWI) ambapo amesema michezo hiyo sio hiari bali ni lazima kwa Watumishi wa Umma nchini

Ametumia fursa hiyo kuwataka Makatibu Wakuu pamoja na  Makatibu Tawala  kuacha kudharau michezo  hiyo huku akisisitiza kuwa michezo hiyo  ipo kisheria.

Amesema michezo hiyo ni muhimu mbali ya kuimarisha afya kwa watumishi wa umma pia inawasaidia watumishi hao kuondoa msongo wa mawazo.

Kufuatia hatua hiyo Mhe, Simbachawene amewataka Watumishi hao walioshiriki michezo hiyo  wakaoneshe utofauti mahali pa kazi ili kuendelea kuipa heshima michezo hiyo ili kuendelea kuwashawishi waajiri wao   kutenga bajeti ya ushiriki  

 

Katika hatua nyingine, Mhe. Simbachawene amewataka Watumishi hao kushiriki uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambapo amesema ushiriki wao ni muhimu sana kwa ajili ya mustakabali wa taifa endelevu.

 

‘’Watumishi walio wengi wanaona kujiandikisha na kushiriki kupiga kura hususan uchaguzi wa Serikali za  Mitaa ni kama  kupoteza muda na sio hadhi yao,nawaomba sana mshiriki kwenye uchaguzi huu.Mhe. Simbachawene amesisitiza

Amesema suala la uchaguzi wa viongozi ni jukumu la wananchi wote wakiwemo Watumishi wa Umma

Naye, Mwenyekiti wa SHIMIWI Daniel Mwalusamba amesema jumla ya Watumishi 2995 wameshiriki kwenye michezo hiyo mwaka huu

Aidha, ametumia fursa hiyo kuwashukuru Viongozi mbalimbali waliojitoa kwa hali na mali katika kuhakikisha mashindano hayo yanafanikiwa