Habari
MHE. SIMBACHAWE AITEMBELEA FAMILIA YA HAYATI MSUYA. YAISHUKURU SERIKALI KWA USHIRIKIANO TANGU ENZI ZA UHAI WA BABA YAO MPAKA KIFO CHAKE

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene ametoa wito kwa Watanzania kumuenzi aliyekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Mzee Cleopa David Msuya kwa kuendelea kudumisha umoja, amani na mshikamano na kuyaenzi mazuri yote aliyoyafanya enzi za uhai wake.
Mhe. Simbachawene ameyasema hayo leo tarehe 22 Mei, 2025 alipoitembelea familia ya Hayati Msuya nyumbani Upanga jijini Dar es Salaam.
Mhe. Simbachawene amesema Hayati Mzee Msuya atakumbukwa kwa kuwagusa watu wengi kwa namna alivyokuwa na upendo, kuwasaidia watu wengi pamoja na kuhamasisha maendeleo katika maeneo mbalimbali nchini.
Aidha, Mhe. Simbachawene amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwathamini Viongozi Wakuu wa Kitaifa Wastaafu kwa mujibu wa Sheria.
Akiongea kwa niaba ya familia, mtoto wa Hayati Msuya, Bi. Joyce Msuya-Mpanju ameishukuru Serikali kwa mchango wake mkubwa na ushirikiano uliotolewa kwa familia hiyo tangu enzi za uhai wa Baba yao alipoanza kuugua hadi umauti ulipomkuta na kusimama bega kwa bega wakati wa msiba mpaka kukamlisha salama taratibu za mazishi yake.
“Tunaishukuru sana Serikali kwa kuwa pamoja na familia yetu tangu Mama alipofariki mmekuwa na Baba bega kwa bega, hii ilisaidia sana hata kumfanya Baba aishi maisha marefu maana tunaelewa mtu anapofiwa na Mwenza hali inavyokuwa. Mhe. Waziri tunaomba utufikishie salamu zetu kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samila Suluhu Hassan, Viongozi wote wa Serikali na Ofisi unayoiongoza kwa upendo mliotuonesha kwetu,” Bi. Joyce ameongeza.
Hayati Cleopa Msuya alifariki dunia tarehe 7 Mei, 2025 na kuzikwa nyumbani kwake Kijiji cha Chomvu, Usangi Wilayani Mwanga Mkoani Kilimanjaro tarehe13 Mei, 2025.