Habari
MHE. SANGU ASEMA SIO HIARI KUTUMIA MFUMO WA e-UTENDAJI KAZI NA KUZINGATIA MAADILI KWA WATUMISHI

“Mfumo wa Kupima Utendaji Kazi kwa Watumishi wa Umma (e-Utendaji kazi) ni matokeo ya maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na ni utekelezaji wa Sheria, Kanuni na Taratibu za Utumishi wa Umma, hivyo ni lazima kila mtumishi wa umma kujiunga na kutumia mfumo huo na si hiari” amesisitiza Mhe. Sangu.
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais UTUMISHI na Utawala Bora Mhe. Deus Sangu ameyasema hayo leo tarehe 15 Agosti, 2024 wakati alipokuwa akifuatilia mawasilisho mbalimbali ya majukumu ya Idara ya Usimamizi wa Mikataba ya Utendaji Kazi Serikalini, Idara ya Usimamizi wa Maadili, Idara ya Usimamizi wa Huduma za TEHAMA Serikalini na Idara ya Mipango ikiwa ni sehemu ya kujifunza kuhusu majukumu ya Ofisi yake.
Mhe. Sangu ameelekeza Idara ya Usimamizi wa Utendaji Kazi Serikalini kufuatilia watumishi wote wa umma mahali popote walipo ili kujua wanafanya nini na kwa maslahi ya nani.
Aidha, ametoa rai kwa idara hiyo kufanya utafiti na kubaini taasisi ambazo zinasuasua kutumia mfumo huo ili hatua za kinidhamu ziweze kuchukuliwa dhidi ya Maafisa Maasuli na watumishi wa Taasisi hizo.
Kwa wakati mwingine ameelekeza Idara ya Usimamizi wa Maadili kutoa mafunzo ya maadili kwa watumishi wapya na walio kazini ili waweze kutambua na kujikumbusha misingi ya maadili katika utumishi wa umma.
“Kuna mambo yasiyofaa ambayo yako kinyume na maadili ya Utumishi wa Umma na yanaendelea katika ofisi za umma kutokana na watumishi hao kujisahau na kuzifanya ofisi hizo kuwa binafsi.
Hali kadhalika, ameipongeza Idara ya Huduma za TEHAMA Selikani kwa kubuni, kusanifu na kutengeneza mifumo ambayo inasimamia utendaji kazi katika utumishi wa umma.
Mhe. Sangu ameendelea na ratiba yake ya kujifunza kuhusu majukumu ya idara mbalimbali zilizopo katika ofisi yake yanayofanyika katika ukumbi mdogo wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mtumba Jijini Dodoma.