Tanzania emblem

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Habari

KAPINGA AHIMIZA WATUMISHI WA UMMA KUTUMIA KUWEKEZA KUPITIA MFUMO WA e-WEKEZA


Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Cyrus Kapinga, amewahimiza watumishi wa umma nchini kujenga utamaduni wa uwekezaji kwa kutumia mfumo wa e-Wekeza kwa kuwa ni mfumo salama na wenye uwazi katika uwekezaji unakuza kipato.

Bw. Kapinga ametoa wito huo leo, Julai 27, 2026, wakati wa mafunzo ya kila Jumatatu yanayoandaliwa na Ofisi hiyo na kufanyika katika eneo maalum la mafunzo Mtumba, Jijini Dodoma.

Bw. Kapinga aliongeza kuwa uwekezaji ni nguzo muhimu ya kujenga ustawi wa kifedha wa mtumishi wa umma, hivyo ametoa rai kwa kila mtumishi wa umma  kutumia fursa zilizopo ili kuweka akiba, kuongeza kipato na uwezo wa kukabiliana na changamoto za kiuchumi zinazoweza kumfanya mtumishi kushindwa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

 “Ni muhimu kwa mtumishi wa umma kujenga tabia ya kuwekeza mapema na taratibu  kupitia mfumo wa e-Wekeza ili kuimarisha ustawi wa kifedha,” alisema Bw. Kapinga.

Bw. Kapinga amesema matumizi ya teknolojia kupitia mfumo wa e-Wekeza yameondoa vikwazo vilivyokuwa vinawakabili wawekezaji wengi kwa kuwawezesha kupata huduma za uwekezaji mahali popote walipo bila kulazimika kufika katika ofisi za taasisi husika.

Kwa upande wao, wataalamu kutoka Watumishi Housing Investments (WHI), ambao ndio wasimamizi wa mfumo wa e-Wekeza, walieleza kuwa mfumo huo umeundwa ili kurahisisha ushiriki wa watumishi wa umma katika uwekezaji kwa njia ya kidijiti.