Tanzania emblem

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Habari

WAZIRI SIMBACHAWENE: SERIKALI YA TANZANIA INAHITAJI VIONGOZI WA KIMAGEUZI KATIKA KUSIMAMIA SHUGHULI ZA MAENDELEO


 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene amesema Serikali ya Tanzania katika kufikia malengo yake inahitaji viongozi wa kimageuzi wenye sifa, weledi na uwezo wa kuongoza kimkakati katika kusimamia shughuli za maendeleo ya nchi.

 

Akizungumza leo Ijumaa Mei 16, 2025 Jijini Dar es Salaam katika Mahafali ya Nane ya Programu za Uongozi zitolewazo na Taasisi ya UONGOZI, Mhe. Simbachawene amesema, uongozi bora ni nguzo ya Maendeleo Endelevu ya nchi huku akisisitiza kuwa hili litafanikiwa kwa kuwa na mikakati thabiti ya kuwajenga na kuwaendeleza viongozi. 

 

Amebainisha kuwa mikakati ya pamoja na kuwa na programu maalumu za kuendeleza viongozi wa ngazi za juu na wanaochipukia katika sekta ya umma, sekta binafsi na Asasi zisizo za Kiserikali ni jambo lisiloepukika.

 

Aidha Mhe. Simbachawene ameipongeza Taasisi ya UONGOZI kwa kuanza maandalizi ya kuwa na programu maalumu ya kuwezesha viongozi chipukizi ambao ni viongozi muhimu sana kwani wana kipindi kirefu cha kulitumikia taifa.

Amefafanua kuwa, kuwandaa na kuwajenga mapema viongozi hao chipukizi  kutaisaidia Serikali kuwa na kundi la viongozi ambao wanaweza kupatikana pale watakapohitajika kuhudumu katika nafasi mbalimbali za uongozi.

 

Kufuatia hatua hiyo, Mhe.Simbachawene amesema Agenda ya Umoja wa Afrika ya Mwaka 2063 itaweza kutimia kwa kuwa na viongozi makini na wenye kujenga Bara la Afrika lenye taswira bora zaidi yenye maono kwa kupunguza vikwazo vinavyorudisha nyuma maendeleo ya Bara hilo.

 

Awali, Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya UONGOZI, Bw. Kadari Singo, amesema programu zinazotolewa na Taasisi hiyo ni mahsusi katika kuwaanda na kuwajenga viongozi ili wakalete mapinduzi mahali pa kazi 

 

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Taasisi ya UONGOZI, Katibu Mkuu Kiongozi Mstaafu, Balozi Ombeni Sefue, amewataka Wahitimu hao wakawe chachu ya kuleta mabadiliko na kuhamasisha uvumbuzi na kutekeleza sera zinazokuza maendeleo jumuishi na endelevu ya Bara la Afrika kwa ujumla.

 

"Tanzania inawahitaji, Afrika inawahitaji na Dunia inawahitaji, nendeni huko mkaoneshe kwa vitendo mlichojifunza kwenye Taasisi ya UONGOZI" amesisitiza Mhe. Balozi Sefue.