Tanzania emblem

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Habari

BODI YA TPSC YATAKIWA KUIMARISHA NIDHAMU NA KUHIMIZA UBUNIFU


Usimamizi bora wa rasilimali, uimarishaji wa nidhamu na uadilifu katika utendaji kazi, kuhimiza ubunifu na kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia ni masuala msingi katika ukuaji wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC)”.

Ujumbe huo umetolewa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw. Juma Mkomi leo tarehe 29 Septemba, 2025 jijini Dar es Salaam wakati akizindua Bodi mpya ya Ushauri ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania.

Aliwaasa Wajumbe wa bodi kutengeneza mazingira ya ushirikiano kati yao, Menejimenti na wadau wote wa chuo ili kuhakikisha mipango ya chuo inatekelezwa kwa ufanisi.

Aidha, Bw. Mkomi aliongeza kwa kuitaka bodi hiyo kutafsiri maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye imejidhatiti kuimarisha uwajibikaji, uwazi, uzalendo na ushirikishwaji katika utendaji wa taasisi zote za umma nchini.

“Ninawaomba mtumie ujuzi, ubunifu na maadili ya Utumishi wa Umma katika kutekeleza majukumu yenu ili kulinda maslahi ya Chuo na Taifa kwa jumla” alisema Bw. Mkomi.

Bw. Mkomi aliongeza kuwa, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora iko tayari kushirikiana na Bodi katika kutekeleza jukumu lake la kusimamia chuo, kutoa dira, mwongozo na ushauri kwa Waziri mwenye dhamana ya Chuo hicho ili kutoa huduma bora.

Naye, Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Chuo hicho, Dkt. Florens Turuka aliishukuru Serikali kupitia Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora kwa kuimarisha miundombinu ya chuo na sasa chuo kinatoa elimu katika mazingira salama.

Dkt. Turuka alimshukuru Katibu Mkuu huyo kwa kuzindua bodi na aliahidi kuwa bodi hiyo mpya itatekeleza majukumu waliyopatiwa kwa ufanisi ili kuleta tija kwa chuo na Taifa kwa jumla.

Awali, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, Dkt. Ernest Francis Mabonesho alisema Chuo hicho kimekuwa kikiwaandaa Watumishi wa Umma kuanzia wanapoajiriwa kwa kuwafanyia Mafunzo ya Awali, Mafunzo Elekezi, Mafunzo ya Umahiri, Mafunzo ya Misingi ya Utumishi wa Umma, Mafunzo ya Uongozi pamoja na Mafunzo ya kuhitimisha Ajira.

Aliongeza kuwa uwepo wa bodi hiyo mpya utaongeza ufanisi na utekelezaji wa majukumu ya chuo kwa kuwa bodi ina jukumu la kutoa ushauri kuhusu shughuli na utekelezaji wa malengo ya chuo, kutoa ushauri katika mipango yote ya maendeleo, kupitisha mpango kazi na bajeti na kupokea na kujadili taarifa ya chuo ya utendaji kazi na fedha.